For Proofreading, Copy-editing, Substantive Editing of Research or Conference Papers, Reports, Manuscripts, Thesis; call: +255 716 23 1772 or E-mail: jaba@udsm.ac.tz

Amani Tanzania

Leo tunayofuraha, kuitwa watanzania,
Kwa amani twatukuka, hata nje ya mipaka,
Mazingira yasifika, wageni yawavutia,
Nchi ya kiafrika, ya watu wenye hamasa,
Tusichezee amani, kwenye shimo la choo.

Ona Rwanda na Burundi, amani waitamani,
Hawataki ukimbizi, wapenda pia amani,
Tuepuke uchochezi, wa kuleta tafurani,
Takayoleta Tsunami, kututenga na amani,
Tusichezee amani, kwenye shimo la choo.

Tushukuru waasisi, wa hii yetu amani,
Kambarage tumuenzi, pia Mzee Amani,
Mola hatotubariki, kama hatuwakumbuki,
Walitoa jasho jingi, amani kuiasisi,
Tusichezee amani, kwenye shimo la choo

Elewa neno ‘amani’, kinyume chake ni ‘vita’,
Gharama yake ni kali, ukitaka irudisha,
Kama huwezi amini, nenda Kongo kuuliza,
Hebu fikeni Sudani, na angaza Liberia,
Tusichezee amani, kwenye shimo la choo.

Vita kama tindikali, katika nyingi jamii,
Taparaganya uchumi, kwongeza umasikini,
Kila siku mafichoni, bila ya kwenda kazini,
Mzalendo tafakari, kabla ya tafrani,
Tusichezee amani, kwenye shimo la choo.

Mito tiririke maji, sipendi kuona damu,
Waafrika jamani, kunani huko Ikulu?
Vita chanzo chake nini, madaraka ndiyo chachu?
Twiga semeni amani, nisingependa vulugu,
Tusichezee amani, kwenye shimo la choo.

Uchaguzi utafika, yetu demokrasia,
Siyo bola kuchagua, chagua aliye bora,
Wengi twamuomba mola, atupe aliye bora,
Amani kuidumisha, ije kuwa yake dira,
Tusichezee amani, wenzetu wanaisaka.

Tuondoe tofauti, ziletazo utengano,
Tubaini wanafiki, wenye uchu na mizozo,
Vichwani wajaza chuki, ubabe na malumbano,
Hakika ni mamluki, waletao migongano,
Tusichezee amani, wenzetu wanaisaka.

Ni vyema nchi wahame, wasotutakia mema,
Wasifanye tukosane, amani kutuponyoka,
Vibaraka waondoke, nia yao siyo njema,
Wenye chuki wapatane, kutuepushia vita,
Tusichezee amani, wenzetu wanaisaka.

Nchi yangu Tanzania, duniani wasifika,
Neema nakuombea, Amani kuimarika,
Wenye hila kupotea, bila damu kumwagika,
Migogoro kufagia, utuliu kuchipuka,
Tusichezee amani, wenzetu wanaisaka.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

0 comments:

Post a Comment