Saa rangi yako nyeusi,
Ngozi yangu mnarandana,
Hukuundwa kwa almasi,
Bali umejengwa kwa nta,
Mlio wako maridhawa,
Damu yangu mmepatana,
Nikwonapo wanikonyeza,
Kisha waniambia muda.
Usiku ninaposinzia,
Waendelea kuzunguka,
Wasaa unapowadia,
Wanitekenya masikio,
Heshima unanitunzia,
Nisichelewe ofisini,
Betri nakuzawadia,
Kwa mwenendo wako mzuri.
Saa tuwapo matembezini,
Hakika ninajiamini,
Rafiki uliye mkweli,
Kila ninapokuhitaji,
Nikuvaapo mkononi,
Rohoni nahisi faraja,
Tuko sote kila mahali,
Wachangia mfanikio
Mwenzio ninakuhusudu,
Ni mengi umenitendea,
Unaniamsha kitandani,
Shughuli kuzipangilia,
Muda unaponitajia,
Ninajibidisha zaidi,
Sitokuachia daima,
Popote tutaambatana.
Saa unanitaarifu,
Shughuli za kutwa zatosha,
Ninapowasili nyumbani,
Ukutani umening’inia,
Umbile lako mduara,
Tik-tok wajizungusha,
Nami macho nakutupia,
Nikiwaza yaliyopita.
Mara waipiga alamu,
Kuna jambo wanikumbusha,
Nakujibu kwa tabasamu,
Mezani nikijisogeza,
Kuchovya inanilazimu,
Pasipo kufanya ajizi,
Kweli saa unanijali,
Ingawa umenigharimu!