For Proofreading, Copy-editing, Substantive Editing of Research or Conference Papers, Reports, Manuscripts, Thesis; call: +255 716 23 1772 or E-mail: jaba@udsm.ac.tz

Siku ya Wapendanao Mpwapwa


MPWAPWA sehemu nzuri, yenye upepo mwanana,
Ukichunguza mandhari, milima inapishana,
Kipindi cha hadhuhuri, mvuto waonekana,
Penye wengi pana mambo.

Tukiwa Mpwapwa shule, vijana tulikutana, 
Na WAGUMU tupo pale, kisera tunapatana,
WALAINI vile vile, wa kike kwa wavulana,
Penye wengi pana mambo.

Ngoja niwapeni kisa, cha WALAINI watatu,
Vijana wana Usasa, wakipigana viatu,
Pasipo kutoa posa, shule mihula mitatu,
Penye wengi pana mambo.

Ni wavulana wawili, kwa msichana mmoja,
Japo watokea mbali, twasoma nao pamoja,
Kwa binti wako chakali, wote kidato kimoja,
Penye wengi pana mambo.

Wa kike jinale Gati, Mzuri wa Wastani,
Mboji na mwenzie Joti, binti wakamtamani,
Wakayapiga magoti, awaumiza rohoni,
Penye wengi pana mambo.

Joti kwao kwenye jiji, ufukara wamkwaza,
Mwenzake kijana mboji, kifedha alijiweza,
Hakusita ‘kuzifoji’, mrembo kumlegeza,
Penye wengi pana mambo.

Wote wakamtongoza, Gati hakuwakataa,
Nasi tulipochunguza, binti kawapa ridhaa,
Mmoja katueleza, mototo anatamaa,
Penye wengi pana mambo.

Penzi lao likadumu, wakiwa naye sambamba,
Watesa nae kwa zamu, japo kawafunga kamba,
Hawakuwa kwenye damu, ingawa hawakuyumba,
Penye wengi pana mambo

Tukafanya utafiti, binti ana lake jambo,
Eti alipenda Joti, sababu ya lake umbo,
Mboji kupendewa noti, na dada huyo mrembo,
Penye wengi pana mambo.

Wawili awachanganya, pasipo wao kujua,
WAGUMU tukawakanya, japo walitutimua,
Kimwana awadanganya, bila ya kujigundua,
Penye wengi pana mambo.

Gati ndumila kuwili, penzini kawanasa,
Waume wote wawili, pasipo kujitikisa,
Kikawa kitendawili, nani talamba galasa?
Penye wengi pana mambo.

Mwezi wa pili ukaja, tarehe kumi na nne,
Ni yupi wawe pamoja, siku ya jumanne,
Gati hana ujanja, kipindi cha saa nane,
Penye wengi pana mambo.
   
Siku ya siku mefika, naona nyekundu nguo,
Vijana wamepambika, kwa mavazi ya kileo,
WAGUMU twataabika, SIKU YA WAPENDANAO,
Penye wengi pana mambo

Sote twaweka mkazo, kwake Gati na vijana,
Nani tapewa likizo, WAGUMU twaulizana,
Leo ni kielelezo, siri itajulikana,
Penye wengi pana mambo.

Mboji mpenda kimwana, Ua akamletea,
Njiani akamwona, Joti memkumbatia,
Kajiumbua kimwana, bwenini kajifungia,
Penye wengi pana mambo.

Gati atia huruma, wamwona kama makapi,
Alidhani lelemama, kuwafanya wao pipi,
Waswahili walisema, njia ya mwongo ni fupi!,
Penye wengi pana mambo.

Hawa vidume wawili, hawakukata tamaa,
Wakabadili kauli, penzi wakalifufua,
Mtoto kawakubali, WAGUMU tukaduwaa!
Penye wengi pana mambo.

Nazo siku zikaenda, twaelekea hitimu,
Wakaanza kujiwinda, kwa nafasi ya kudumu,
Kimwana wakamganda, sawa na wendawazimu,
Penye wengi pana mambo.

Yakafika mahafali, nani atavishwa taji?
Gati kajificha mbali, katika pembe ya mji,
Ni Joti mara ya pili, kumzidi Kete Mboji!,
Penye wengi pana mambo.

Jambo likazua mambo, Mboji anaweweseka,
Mwenzetu kakosa pambo, japo alighalimika,
Gati kategua fumbo, kwa Joti amezimika!.,
Penye wengi pana mambo.

Mwisho Mboji kasadiki, kweli penzi siyo pesa,
Mtoto hakamatiki, hatimaye kamkosa,
Sasa imekuwa chuki, Gati pesa katakasa,
Penye wengi pana mambo.

Twashukuru mtihani, kwa kumaliza mzozo,
Yao macho vitabuni, wakasitisha mchezo,
Wote ‘bize’ masomoni, mtihani ndo kigezo,
Penye wengi pana mambo.

Tukahitimu cha sita, sote tukatawanyika,
Penzi lapata utata, mme mwenza karidhika,
Joti naye anasota, Gati ameshatoweka,
Penye wengi pana mambo.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Kizunguzungu


Nami leo nalo swali, naomba mnipe jibu,
Nataka kupata mwali, tabia yake dhahabu,
Najaribu kusahili, lakini sina jawabu,
Mie nimpende nani, na kwanini nimpende?

Katika jamii yetu, wapo wengi wasichana,
Tabia zao za chatu, hawapendi kutafuna,
Wengi wao watukutu, wana wengi mabwana,
Mie nimpende nani, na kwanini nimpende?

Nataka Binti mweusi, nashangaa simpati!,
Japo waishi na sisi, wajifanya tofauti,
Uzuri wa mkakasi, ndani kipande cha mti,
Mie nimpende nani, na kwanini nimpende?

Wapo wenye mikorogo, utadhani waasia,
Wajipanga mlolongo, saluni kujipodoa,
Wengi wao ni waongo, wahitaji wenye nia,
Mie nimpende nani, na kwanini nimpende?

Mavazi yanichukiza, nusu uchi wanavaa,
Miili wanaiuza, utadhani ni vichaa,
Mi bado najiuliza, wanatafuna milaa,
Mie nimpende nani, na kwanini nimpende?

Nikioa kijijini, ‘aweza-chenji’ mjini,
Na akawa limbukeni, wakunitia shidani,
Wenye mali kutamani, penzi kuwa kitanzini,
Mie nimpende nani, na kwanini nimpende?

Na hao wa geti-kali, naogopa kudekewa,
Pia kuzibwa kauli, na shidani kukimbiwa,
Kwani palipo ukweli, uongo utenguliwa,
Mie nimpende nani, na kwanini nimpende?

Msomi ningetafuta, lakini ni wasumbufu,
Watembeapo hunata, na wapenda kujisifu,
Mali mtakapopata, hujiona wakamilifu,
Mie nimpende nani, na kwanini nimpende?

Meangaza duniani, bado sijapata wangu!
Japo mwili watamani, roho yaweka kiwingu,
Hakika nimeamini, mapenzi kizunguzungu!
Mie nimpende nani, na kwanini nimpende?

Kumbuka mie fukara, wengi wanataka fedha, 
Nami na pesa uchwara, kuishi nao ni adha,
Penzi lisije nikera, ninaomba mawaidha,
Mie nimpende nani, na kwanini nimpende?

Tambua mie mgumu, sipendi wakunitenda,
Nisijepatwa wazimu, na kuapa kutopenda,
Nikaja kukosa hamu, mapenzi kutoyapanda
Mie nimpende nani, na kwanini nimpende?

Mapenzi yanitatiza, kaka yenu sijiwezi,
Warembo wanikonyeza, ninahisi wapuuzi,
Fikra zanikataza, je niachie wazazi?
Mie nimpende nani, na kwanini nimpende?

Nimebaki njia panda, sioni wakumpenda,
Kila ninaemuwinda, moyo wangu wamponda,
Miaka mbio yaenda, nani moyo taushinda?
Mie nimpende nani, na kwanini nimpende?

Kirika nashawishika, kujitia mawindoni,
Kabla sijapotoka, zenu nasaha toeni,
Kalamu naitundika, yetu mawazo nipeni,
Mie nimpende nani, na kwanini nimpende?

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Maajabu


1. Chunga wako mdomo,
    Uombao kila kitu,
    Walowahi omba na kuonja,
    Hawasiti kusifia,
   Yao kiu wamekata,
    Kwa maji ya ajabu,
    Maji hayo asilia,
    Chemichemi adimu,
   Yapo tokea enzi,
   Wenye ndevu huyateka.

2. Vitu vingi tumeonja,
    Hata visivyohesabika,
   Vyenye utamu wa asali,
   Na uchungu wa shubiri,
   Pia vyenye ukakasi,
   Na vilosheheni uchachu,
   Hebu swali jiulize,
   Radha ipi ni bora?

3. Katikati ya nyika,
   Yenye miti miwili,
   Kuna kisima cha ajabu,
   Chapakana na milima,
  Kingo zake raini,
  Kila wakati zagongana,
  Juu yake kuna nyasi,
  Maji yake mruwa,
  Wenye kata huyateka.

4. Nusu mita toka kisimani,
    Pana matunda mawili,
   Yalosimama wima,
   Mithili ya vichuguu,
  Yote yatoa unyevu,
  Majira ya masika,
  Pembezoni mwa kisima,
  Pana sehemu tambarare,
 Maji yanapopampiwa,
 Cha ajabu pafurika!

5. Nyasi ndefu zafyekwa,
    Kisima wazi mwituni,
   Kikingojea watekaji,
   Kiu yao kuikata,
   Utamu usoelezeka,
  Heko jalali kukiumba,
  Kisima kisichonyauka,
  Toka zama za mababu.

6. Wamiliki wa kisima,
    Hakika wana masharti,
    Kuonja yake maji,
    Mpaka uwe na pampu,
   Tena iliyo imara,
   Kisimani utumbukize,
   Pumzi ukishindilia,
   Uvute maji matamu,
   Lo! Kisima hiki cha enzi,
   Koho laburudika!

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Tausi


Nimezunguka mwituni, pasipo kutarajia,
Na sikuwa mawindoni, basi ndege kanijia,
Jinale tausi-jani, mwenyewe kanitajia,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Nikachunguza umbole, likanitia wazimu,
Sikuwahi penda kale, huyu ndege muhimu,
Nimeandaa mishale, kumtupia kwa zamu,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Ewe tausi mrembo, kweli umependelewa,
Nionapo lako umbo, hakika umejaliwa,
Kichwani bado ni fumbo, ni wapi umezaliwa?
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Tausi ndege mzuri, mrembo wa kuvutia,
Wang’aa kama Hariri, mwanga waniangazia,
Mwangaza wa kibatari, tena usiofifia,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Shingo mithili ya twiga, yavuta kama sumaku,
Mboni zako za kichaga, ni sawa na za chiriku
Mwendo wako wa kinyonga, wazidisha dukuduku,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!
Katika kundi la ndege, wewe ndiye malkia,
Hata kanga wakuige, robo hawatofikia,
Mikorogo wakoroge, rangi yako asilia,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Sauti yako nyororo, kama nyuzi za gitaa,
Mie napata kihoro, sawa na giza kwa taa,
Tujifunge minyororo, tupite kila mtaa,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Mzuri mwenye adabu, vijana wakutafuta,
Japo huvai dhahabu, kizani wameremeta,
Mvuto wako dhawabu, upweke utanifuta,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Mlimbwende wa dunia, mabawa ya almasi,
Macho nikikwangazia, wewe ni lulu tausi,
Hakika nimepania, hebu toa wasiwasi,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Mawazo ni kimbiliyo, yadhihirisha bidii,
Tabia uliyonayo, yanivuta kwa utii,
Kwako nitasema ndiyo, uwamuzi sijutii,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Nisemacho ni sahihi, na wala siko peponi,
Moyo wangu wafurahi, kwa yako rangi mwilini,
Nikwonapo asubuhi, najihisi burudani,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Jinsi unavyorembua, wanifanya niwe hoi,
Tausi wanisumbua, japo siri sitoboi,
Yakubidi kutambua, ngozi yako kama toi,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Kichwa chazidi niuma, mwenzio sina ruzuku,
Upitapo nainama, mwenzako mie kasuku,
Kisha najishika tama, usinitoe mkuku,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Mtima wafadhaika, kwangu ua waridi,
Ninashindwa kutamka, japo sipendi kuwadi,
Midomo yatetemeka, sipati hoja jadidi,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Tuwe sote mawinguni, unaporuka hewani,
Tuitunze bustani, ua lichipue chini,
Kisha nione usoni, penzi latoka moyoni,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Kila tunapokutana, macho tunakaziana,
Kihisia twapendana, kunena twaogopana,
Mikono tukishikana, twaduwaa kuachana,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Sitaki nimtizame, anifanye nikumbuke,
Naye hataki nihame, roho isifadhaike,
Penzi ni kama umeme, ushikapo nyaya zake,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Anipigia kinanda, kihisia niko kati,
Mawazo yarandaranda, napo panga mikakati,
Sasa niko njia panda, japo napenda kwa dhati,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Nampenda maradufu, nataka awe wa kwangu,
Penzi ni kama upofu, mbele naona ukungu,
Rohoni ninayo hofu, nahisi kizunguzungu,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Napokuona usoni, kuna jambo walificha,
Nipe yaliyo rohoni, pendo lisije kuchacha,
Nong’oneze sikioni, nikufanye wangu kocha,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Mtima umeushinda, haunalo pingamizi,
Tazama nilivyokonda, mithili ya sisimizi,
Sababu ninakupenda, na sipendi kuwa wazi,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Tuweke wazi hisia, milele tuwe pamoja,
Mashoga kuwasusia, pendo lisije kuchuja,
Kuzingatia wosia, iwe ngao ya vihoja
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Unipende tupendane, tusendelee fichana,
Nasi tukubaliane, pasipo haya kuona,
Popote tushikamane, kama mapacha vijana,
Kuwa nawe natamani, ingawa mie mgumu!

Naomba nitamkie, uniondoe shidani,
Watu wote watambue, tumeungana rohoni,
Hisia tuzifichue, tutaficha mpaka lini?
Najua tunapendana, tuweke hisia wazi!

Mara ndoto yanijia, pamoja tuko peponi,
Pete wanizawadia, na kunibusu shavuni,
Nami nakukumbatia, na kuvisha kidoleni,
Tuifanye ndoto kweli, popote tuambatane.

Twaogelea bwawani, jua latoa miali,
Furaha tele rohoni, naona kitendawili,
Katika mabilioni, tumesimama wawili!
Oooh tausi mzuri, wewe ni Ua waridi.

Tazama bustanini, Ua pendo lachanua,
Kulichuma natamani, macho waniangazia,
Mwenzio sioni soni, moyo umekuchagua,
Mawazoni ndiwe nyota, tokea alfajiri.

Hebu nione machoni, kuna upendo wa dhati,
Nitazamapo pichani, kifikra huwa kati,
Ni wewe tu duniani, meniteka kwa manati,
Niruhusu nikupende, ndoani tuwe mfano.

Tausi macho yafunge, kurasa mpya fungua,
Dengua kwa vitatange, penzi kutolitengua,
Warembulie vingunge, hila zao kupangua,
Liruhusu pendo langu, doani tuwe mfano.

Tausi kakamilika, mvuto wa kimahaba,
Akipita nagutuka, kaniganda kama ruba,
Nikimwona nazimika, analo jicho la huba,
Ingawa mie mgumu, hisia umeziteka!

We kidani cha nafsi, wengine sina nafasi,
Ingawa wananighasi, Waarabu kwa watusi,
Hawanipi wasiwasi, nimekupenda tausi,
tokea alfajiri, Mawazoni ndiwe nyota.

Zivae zako chachandu, ujivike na ushungi,
Shanga zako za kihindu, zanikuna mara nyingi,
Mboni zako za utundu, kama binti wa kirangi,
Liruhusu pendo langu, ndoani tuwe mfano.

Unikunapo kidevu, nahisi nina bahati,
We sehemu ya ubavu, sina tena kizingiti,
Tuwe sote nchi kavu, tupae kwa parachuti,
Ingawa mie mgumu, hisia umeziteka!

Tausi waniumiza, mwili wautetemesha,
Kutwa nzima kukuwaza, mtima wautonesha,
Macho unavyolegeza, Urembo wauboresha,
Ingawa mie mgumu, hisia umeziteka!

Nasi tuwe wawazi, tangazo kwenye mimbali,
Upendo wa wiziwizi, waipunguza morali,
Tufahamishe wazazi, ili watupe kibali,
Tuwe mithili ya njiwa, anga wawiliwawili.

Kanisani tufichue, huku twavuta subira,
Hata rafiki wajue, rohoni ndiwe kinara,
Ndugu nao watambue, pete itoe ishara,
Tuwe mithili ya njiwa, anga wawiliwawili.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS