For Proofreading, Copy-editing, Substantive Editing of Research or Conference Papers, Reports, Manuscripts, Thesis; call: +255 716 23 1772 or E-mail: jaba@udsm.ac.tz

Fimbo


Ngoja nianze kwa kisa, kilichonifika mie,
Ni washuleni mkasa, ngoja niwasimlie,
Najua mnahamasa, naomba msisinzie,
Pole nitao wagusa, tena mnivumilie
Kwanza tukubaliane, ni Ukweli na Uwazi

Kokoriko! Naamka, nawaza kwenda shuleni,
Kwa-kwa! Shule nimefika, ngo-ngo! Wote paredini,
“mbona wewe unacheka, hebu lala sakafuni”,
Mwili wanisisimka, napo chapwa matakoni,
Kha! Maisha ya shuleni, kweli ni safari ndefu.

Mara vipindi vyaanza, wanafunzi twashtuka,
Hesabu ndicho cha kwanza, wengi tunahuzunika,
Kabla hatujaanza, bongo zaanza chemka,
Huyu bwana aongoza, kwa viboko kutunyuka,
Hii adhabu ni mbaya, yatutia wasiwasi.

Mwalimu anaingia, fimbo tatu mkononi,
Gafla namchukia, sielewi ni kwanini?,
Labda alichangia, hesabu kutotamani,
Nashindwa kuvumilia, najisikia huzuni,
Hii adhabu si nzuri, yatuvunjia heshima.

Kila siku atuchapa, hesabu kafanya chambo,
Tumwonapo twaogopa, apitako ana fimbo,
Ofisini ajitapa, wote wafate mkumbo,
Katunoa kama tupa, kwa kuyatunga mafumbo
Wengi wamesusa somo, kwa sababu ya viboko.

Leo ametoa swali, na mfano hakutoa,
Wote tumekosa swali, mfanoe hajatoa,
Mara! Fimbo mbilimbili, wote katuzawadia,
Nimefikiria mbali, kwa somo kutolijua,
Wengi wamesusa shule, kwa sababu ya viboko.

Kutoka katika kisa, mengi tumefundishana,
Niliyoeleza hasa, wengi mlishayaona,
Basi tuvipinge sasa, twepushe kudhuriana,
Tusiingize siasa, tukaja laumiana,
Fimbo sumu ya elimu, yapaswa kutokomezwa.

Wote walo watukutu, tiba yao si viboko,
Tawatia ukurutu, mithili ya mbwa koko,
Lakini watadhubutu, baada ya michubuko,
Jamani tujali utu, viboko siyo zindiko,
Fimbo sumu ya elimu, yapaswa kutokomezwa.

Weupe walianzisha, haki zetu kuzibana,
Kwanini tunajishusha, kwa fimbo twaumizana,
Mwendo huu tumekwisha, hatuwezi kufichana,
Mwenzenu zilinichosha, na sitaki kuziona,
Lo! Adhabu ya Viboko, Kasumba ya Kikoloni.

Watoto haki wapeni, tena kwa moyo mweupe,
Hata huko majumbani, viboko tusiwachape,
Wazazi tekelezeni, msifanye waogope,
Walimu tufatieni, zetu fimbo tuzitupe,
Lo! Adhabu ya Viboko, Kasumba ya Kikoloni.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Mwanga (Sehemu ya Pili)


Elimu sawa na Mwanga, ujinga ni kama giza,
Giza linatangatanga, ili mwanga kuumeza,
Vitabu ndiyo uganga, giza vinatokomeza,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Adui yetu ujinga, kazidi kuchachamaa,
Akili katia chenga, mkaa kaipakaa,
Vichwani kuna mchanga, ubongo umechakaa,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Gizani siyo patamu, patufanya tusumbuke,
Mwanga ushike hatamu, kwa wanaume na wake,
Mshike sana elimu, simwache aende zake,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Wananchi mtambue, hili nalowakumbusha,
Giza lisiwakomoe, tamaa kuwakatisha,
Jamii ijikomboe, elimu mwanga wa maisha,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Penye kutetea haki, elimu ni ufunguo,
Bila hata kuhamaki, waweza mipangilio,
Nyuma nyuma hutobaki, kwako mbele ni chaguo,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Wafanyie tathimini, waliopita shuleni,
Mawazo yao makini, tena wanajiamini,
Tazama wanazuoni, mwenyewe utatamani,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Tuliweka azimio, hafe adui ujinga,
Hataki maendeleo, kila mara atupinga,
Simpe upendeleo, mbele twataka kusonga,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Taasisi za elimu, zipo nyingi duniani,
Kusoma iwe muhimu, ili tutoke gizani,
Tuonesheni nidhamu, na bidii mafunzoni,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Tuboreshe mazingira, Taasisi za Elimu,
Tusome bila harara, kuyamudu majukumu,
Elimu iliyobora, kujali ubinadamu,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Mkiwa wataalamu, mwajibike bila mbwembwe,
Japo mapato hadimu, shughuli zitekelezwe,
Nasi wadau wa elimu, tujifungeni vibwebwe,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Tuzidi kuhimizana, ujinga tutokomeze,
Masomo kukumbushna, na mafunzo tumalize,
Elimu mwisho haina, sote tujiendeleze,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Sehemu za kusomea, nazo zikidhi ubora,
Vitendea kazi pia, vyendane na mazingira,
Ujinga kutokomea, tuboreshe mishahara,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Mwanga (Sehemu ya Kwanza)


Kuna giza mbele yangu, japo mie si kipofu,
Nyuma naona ukungu, ninakoenda sihofu,
Japo naonja vichungu, moyo wangu mkunjufu,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Mwendo mithili ya kaa, upande nachechemea,
Gafla ninajikwaa, nanguka kama gunia,
Ubongo umedumaa, giza limeninamia,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Usiku umeingia, njiani ninatembea,
Giza linavizia, nyota zinanizomea,
Mwezi waniangazia, ninazidi kujongea,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Tupo tulio shimoni, hatuoni pa kushika,
Tunapapasa gizani, nuru imeshatoweka,
Yowe twatoa kinywani, ni mwangwi tu wasikika,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

Gizani kuna vitisho, vyatufanya tuogope,
Tufanye matayarisho, kabla ya kuja kupe,
Mwanga usiwe na mwisho, na sote tuwe peupe,
Mwanga wafukuza giza, kutogubika dunia.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Khanga (Sehemu ya Pili)


Malezi kwetu watoto, we mhusika mkuu,
Kwa upendo motomoto, nasaha hali ya juu,
Maishani ni fukuto, twaishi bila makuu,
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.

Khanga mbona wakubana, haki zako zitambue,
Nawe kazini kazana, jua ulivumilie,
Kama ndoa ni ndoana, acha using’ang’anie!
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.

Kwenye pingu za maisha, pingeni kunyanyasika,
Ngumi na fimbo zatosha, msipende sulubika,
Sulubu kukaribisha, na meno yenu kung’oka,
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.

Nanyi shirikianeni, kukwepa dharauliwa,
Kidole cha kiganjani, hakiwezi vunja chawa,
Wanaowaona duni, wanafaa kuzomewa,
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.

Kataa kuwekwa nyuma, usije sahaulika,
Usitake kuinama, wasije wakakuruka,
Roho mithili ya chuma, izidi kuimarika,
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.

Majogoo yamewika, mama-zetu amkeni,
Msipende kubweteka, mbele nanyi simameni,
Bila ya kutetereka, kamateni usukani,
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Khanga (Sehemu ya Kwanza)


Khanga vazi la heshima, limelea weshimiwa,
Ndiyo mbeleko ya mema, kwetu tuliozaliwa,
Kila napokutazama, wafaa kuzwadiwa,
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.

Hakika nimeamini, khanga wavaao bora,
Tabia zao makini, wa visiwani na bara,
Wafanyie tathmini, kivitendo wanang’ara,
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.

Khanga hataki uvivu, afanya shughuli nzito,
Atumia zake nguvu, bila hata ya majuto,
Kazi za ukakamavu, kwake zaleta mapato,
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.

Hakiki maofisini, khanga ndilo vazi hasa,
Tazama wanazuoni, wenye khanga watikisa,
Wachunguze marubani, khanga wavaa kisasa,
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.

Wapitishao amri, wapo wanavaa khanga,
Wafanya kazi vizuri, na hawapendi ujinga,
Wapo pia wahariri, taifa letu wajenga,
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.
Ona kipato cha mji, mwenyewe wakitafuta,
Kilimo kwenye vijiji, peke yako unasota,
Wana watakapo uji, wawapa bila kusita,
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.

Chunguza walo mjini, wanalopata kidogo,
Watangatanga njiani, biashara zao ndogo,
Wauza mboga-majani, bila hata ya maringo,
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.

Tazama mama ntilie, kutwa nzima yu moshini,
Yapasa wavumilie, japo wachuma juani,
Kipato watupatie, wana twende masomoni,
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.

Shughuli mnabebeshwa, wasidhani nyie punda,
Mwapaswa kupumzishwa, na mfaidi matunda,
Msizidi kunyanyaswa, huku miaka yaenda,
Tusikubali unyonge, khanga ndilo vazi letu.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Nguruwe


Kati ya wanyama wote, nguruwe anichefua,
Nashindwa kumeza mate, kila napomwangalia.

Unajua ni kwanini?, kwa sababu ni mchafu!,
Kwake chochote tumboni, si kwamba namkashifu.

Litazame lake zizi, litakutia kinyaa,
Kulisafisha hawezi, mikono imesinyaa.

Tembo watoa amri, wote wachimbe jalala,
Nguruwe hajihadhari, vichafu ndo anakula.

Choo ameishakanywa, zao kelele hachoshwi,
Na maji anayokunywa, hakika hayachemshwi.

Ukianza kuchunguza, hata kichanja hana,
Ila kinachoshangaza, azidi nenepeana!.

Masika yapofika, zizini kipindupindu,
Kuhara na kutapika, kama kameza ukindu.

Hebu mtazame paka, mwenyewe utasifia,
Kwa miguu afunika, alipojisaidia.

Alala juu ya sofa, pasipo kulichafua,
Ulinzi nampa sifa, panya atufukuzia.

Chakula tunachokula, paka atia kinywani,
Paka ingawa kabwela, usafi yuko makini.

Ewe paka mwelimishe, wako ustaarabu,
Usafi umfundishe, hasingoje matibabu.

Nguruwe ona aibu, mwenyewe umebakia,
Ujinga siwe sababu, balaa kujizulia.

Wito wanyama wenziwe, mnaocheza sambamba,
Kiiga kunya kwa tembo, utapasuka msamba!

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Maisha (Sehemu ya Pili)


Safari bado ni ndefu, sijione mtukufu,
Tabia za ushaufu, wenzio zinawakifu,
Ufahari sifa mfu, usipende kujisifu,
Maisha ndivyo yalivyo, kupanda pia kushuka.

Waona tope wenzio, kisa kumiliki gari,
Maisha kikaangio, punguza yako jeuri,
Ulapo vipapatio, sitafune kwa kiburi,
Maisha ndivyo yalivyo, kupanda pia kushuka.

Simcheke mlemavu, hujui mtondogoo,
Jifunze unyenyekevu, sijifanye komandoo,
Ukwasi wakupa nguvu, kudhani wenzio choo,
Maisha ndivyo yalivyo, kupanda pia kushuka.

Kuna watu tegemeo, wana roho ya kwanini!,
Kwani tajiri wa leo, kesho ndiye masikini,
Tuishi kama kondoo, tukafaidi peponi,
Maisha ndivyo yalivyo, kupanda pia kushuka.

Kuna watu wana njaa, wachache wala wasaza,
Wapita kwenye mitaa, waloshiba wakubeza,
Wengi wakata tama, kutwa nzima wanawaza,
Maisha ndivyo yalivyo, kupanda pia kushuka.

Zangu rai nimetoa, mwanadamu jitambue,
Zako kasoro ondoa, wenye shida uwafae,
Umaskini ni doa, jamii ijikomboe,
Maisha ndivyo yalivyo, kupanda pia kushuka.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Maisha (Sehemu ya Kwanza)


Dunia naona chungu, siyo sababu majungu,
Sababu ni walimwengu, kuteta yaliyo yangu,
Kisa mie sina changu, mbele yangu ni ukungu,
Maisha ndivyo yalivyo, kupanda pia kushuka.

Ninayo matumaini, siku moja nitapata,
Japo bado ni kizani, na ndoto zenye utata,
Nazidi omba manani, nami tija kuipata,
Maisha ndivyo yalivyo, kupanda pia kushuka.

Mie ni Mtanzania, lazima niwe na nia,
Maisha kupigania, ingawa wanitania,
Kwamba mie ni ngamia, ndivyo walivyonuia,
Maisha ndivyo yalivyo, kupanda pia kushuka.

Ona watoto yatima, wahitaji misaada,
Kila unachokichuma, simalize na vimada,
Tambua hili mapema, wape masikini ada,
Maisha ndivyo yalivyo, kupanda pia kushuka.

Ombaomba mitaani, msaada watamani,
Wenye nacho mkononi, hebu wasaidieni,
Iwe kutoka rohoni, na mola atawapeni,
Maisha ndivyo yalivyo, kupanda pia kushuka.

Wapo walokuwa juu, hivi sasa wako chini,
Watembea kwa miguu, bila kitu mifukoni,
Nguo zao kuukuu, kujificha watamani,
Maisha ndivyo yalivyo, kupanda pia kushuka.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Jungu Kuu (Sehemu ya pili)


Enyi wana wa mwanangu, nina miaka tisini,
Kufika umri wangu, hakika mnatamani,
Niko kama nungunungu, mwili navyouthamini,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Ndugu wajukuu zangu, lazima mjiamini,
Mnavyoishi kizungu, na magonjwa jichungeni,
Msijemeza vichungu, kutumbukia jangani,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Mfano ni gonjwa hili, la upungufu wa kinga,
Mkiweza lihimili, mwaka wangu mtatinga,
Na hata mia kamili, haita wapiga chenga,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Wajukuu nawasifu, katika hiki kikome,
Shule muwe watiifu, tabia hasi zikome,
Pia muwe wangalifu, na heshima iwe ngome,
Msipende kujisifu, nayo fitina mwichome.

Mwisho ninawakumbusha, nyie taifa la kesho,
Bidii kuionesha, shuleni hisiwe mwisho,
Mifuko kuitunisha, na kuepuka vitisho,
Kumbukeni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Mkizingatia haya, mtaishi kama mimi,
Pasipo kuwayawaya, watawaita wasomi,
Nanyi msiwe na haya, kujenga wetu uchumi,
Kumbukeni jungu Kuu, hakika lina ukoko

Leo ninawashukuru, hamjapiga kelele,
Msiwe kama kunguru, enendeni mkalale,
Mkiwa nao udhuru, njooni kama mshale,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Jungu Kuu (Sehemu ya Kwanza)


Babu yenu nawaita, njooni kwenye kikome,
Niwape yaliyopita, mtoke kwenye Umeme,
Yasije yakawakuta, miaka yenu ni dume,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Enyi wangu wajukuu, hebu nisikilizeni,
Nami nina mambo makuu, nataka niwambieni,
Kwani bado niko juu, na mwenye matumaini
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Hebu nyote tazameni, huu wangu mkongoja,
Umri wawapiteni, msidhanie porojo,
Nina miaka tisini, waniongoza rojorojo,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Huu weupe kichwani, umeona mambo mengi,
Najua mnatamani, kuishi miaka mingi,
Lakini mtambueni, mbele mnavyo vigingi,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Ninyi wadogo kabisa, tena bado mnasoma,
Hamjakumbwa mikasa, kwenu dunia ni njema,
Machoni kuna vitasa, kila mtu kwenu mwema,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.
Naanza waelimisha, wajukuu wasichana,
Vishawishi vya maisha, nyie vya wanasa sana,
Malengo vyapukutisha, mtegoni kuwabana,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Ninyi watoto wa kike, masomo zingatieni,
Mabwana wana makeke, mimba wakiwatieni,
Kila siku mkumbuke, mwajingiza matatani,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Mkiwa bado shuleni, wengi mnawavutia,
Kwa mali wawarubuni, tena wakiwasifia,
Jinasue mtegoni, ili msijejutia,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Wengi wa hao mabwana, matapeli wa mapenzi,
Mkisha kubaliana, umejivisha kitanzi,
Mimba mkitunguana, wanakuona mshenzi,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Shuleni mkifukuzwa, kwa wazazi kitimoto,
Mtaani mtatengwa, hata na hao vizito,
Kwa ndugu mtapuuzwa, mtabaki na majuto,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Mimba umri mdogo, kujifungua tatizo,
Yaenda mbio mapigo, kichwani tele mawazo,
Utakufa kama gogo, na kutwachia gumzo,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Pia mwaweza chanika, pindi mnajifungua,
Na yenu ngao kumbuka, subiri mtapokua,
Ungojee lako rika, masomo mkiripua,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Wajukuu wavulana, nanyi pia nawahasa,
Popote mkikutana, muepukeni hanasa,
Mzidi elimishana, kuachana na usasa,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Zingatieni elimu, na mwache udhururaji,
Sikilizeni walimu, wakuze vyenu vipaji,
Wazazi kuwaheshimu, wa mjini na vijiji,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Kumbuka penzi na shule, kimantiki vyapingana,
Mwapaswa kuona mbele, masomo kufundishana,
Nanyi mfike kilele, mafanikio mwanana,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

Vishawishi vya akili, duniani mvikwepe,
Dawa za kulevya mwili, zisiwafanye mapepe,
Na ngono mzikabili, nchi isiwe nyeupe,
Tambueni jungu kuu, hakika lina ukoko.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Mama Zetu (Sehemu ya Pili)


Mama machozi futeni, ukombozi umefika,
Msiwe viumbe duni, mwazidi kunyanyasika,
Haki zenu hadi lini? Adha yavuka mipaka !
Hawa ndio mama zetu, yatubidi tuwaenzi.

Serikali nazo dini, tuacheni ubaguzi,
Yafaa tuwathamini, kwa kuwapa uongozi,
Vyeo tuwapandisheni, popote ngazi kwa ngazi,
Hawa ndio mama zetu, yatubidi tuwaenzi.

Rai nawapa wazazi, nanyi jirekebisheni,
Zigaweni sawa kazi, na pasipo ukinzani,
Chanzo tofauti hizi, huko huko majumbani,
Hawa ndio mama zetu, yatubidi tuwaenzi.

Enyi wanaharakati, wa mambo ya kijinsia,
Iwekeni mikakati, na acheni kusinzia,
Iwe ni yake tamati, unyanyasaji jinsia,
Hawa ndio mama zetu, yatubidi tuwaenzi.

Manani jicho katupa, sote tulione hili,
Mola sikio kakupa, nisikie mara mbili,
Allah ubongo kawapa, tatueni kwa akili,
Hawa ndio mama zetu, yatubidi tuwaenzi.

Kunywa msema maneno, akili mtoa jambo,
Ya jinsia malumbano, sote tuyaweke ng’ambo,
Sheria ni msumeno, ikate huku na huko!
Na wapewe haki sawa, hawa ndio mama zetu

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Mama Zetu (Sehemu ya Kwanza)


Toka mwanzo wa dunia, mwawaona watu duni,
Ni wachache twajutia, japo hatuna idhini,
Nao wazidi umia, haki zao mashakani,
Hawa ndio mama zetu, yatubidi tuwaenzi

Hasa huku Afrika, mfumo dume wazidi,
Mila zetu zasifika, wa kike kuwakaidi,
Sijui yetu hulka, kubinya ua waridi!,
Hawa ndio mama zetu, yatubidi tuwaenzi.

Wengi wanalazimishwa, ndoa na wasiorika,
Babu zao waodheshwa, bila wao kuridhika,
Kweli mnataabishwa, ni lini mtaboreka?
Hawa ndio mama zetu, yatubidi tuwaenzi.

Kwa upande wa elimu, hawana kipaumbele,
Wa kike mwawadhurumu, ili wasisonge mbele,
Kusoma sasa muhimu, tuachane na ukale,
Hawa ndio mama zetu, yatubidi tuwaenzi.

Wajane waliofiwa, wanyang’anywa mali yote,
Watakiwa kurithiwa, na shemejiye yeyote,
Lini watathaminiwa, moyoni wametemete?
Hawa ndio mama zetu, yatubidi tuwaenzi.

Ugawanaji mirathi, kimila tunawatenga,
Na tena wapo baadhi, wafukuzwa kwa mapanga,
Kisheria wana hadhi, japo mwawapiga chenga,
Hawa ndio mama zetu, yatubidi tuwaenzi.

Wapo mnaowaita, eti mama wa nyumbani,
Wapigwa kila nukta, kama mdundo ngomani,
Tena bila ya kusita, mateke hadi tumboni,
Hawa ndio mama zetu, yatubidi tuwaenzi.

Kwenye soko la ajira, twawabagua kwanini?
Kuwajiri ni nadra, wapewa vyeo vya chini!,
Twasababisha harara, mwenendo tuupingeni,
Hawa ndio mama zetu, mnanitia uchungu!.

Kila tunachokiweza, wao pia wanaweza,
Mbona tunawadumaza, hebu jaribu kuwaza,
Wajuzi twawapoteza, ndilo linaloshangaza.
Hawa ndio mama zetu, yatubidi tuwaenzi.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Kioo (Sehemu ya Pili)


Kuna watu wa ajabu, ukabila hawaachi,
Wavunja utaratibu, japo nao wananchi,
Huu si ustarabu, kama kula nyama mbichi!,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Ofisi wafanya zao, wamo wa kabila moja,
Hawatojali wenzao, wasio toka pamoja,
Kabila lao chaguo, labda huzue hoja,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Roho yao ya umimi, inaturudisha nyuma,
Wenzenu hamtizami, hamna hata huruma,
Ni vizuri mjihami, japo bado mnavuma,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Yupo anayejiweza, mikono yake birika,
Kivipato aongoza, popote aheshimika,
Kuzitoa akiweza, rohoni anung’unika,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Ninapigwa bumbuwazi, sipendi kuitwa duni,
Wapo wenye ubaguzi, waona wenzao nyani,
Kujishusha hawawezi, waweka wenzao chini,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Sisi sote binadamu, weupe ama weusi,
Tusiishi kama ndimu, baadhi kuwa mabosi,
Duniani hatudumu, sote twapita kwa kasi,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Wapo wengi wanatajwa, tabia zao asidi,
Hakika wana magonjwa, waeneza makusudi!
Wenye tamaa waponzwa, wakidhani wafaidi!,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Tazama yako taswira, rohoni ujikosoe,
Ukiweza kujichora, kwa hekima jipodoe,
Tamka neo busara, kisha macho yakodoe
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Kioo (Sehemu ya Kwanza)


Nimekaa kwenye ndoo, huku nimekunja ndita,
Navuta yangu droo, kuna kitu natafuta,
Pembeni kuna kioo, ambacho kinanisuta,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Mwenzenu ninasumbuka, kwa ninachokitazama,
Ninacheka anacheka, nainama ainama,
Gafla nahuzunika, nae ajishika tama,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Tabia za walimwengu, zinanistajabisha,
Wapo wapenda majungu, na wale wenye kubisha,
Nilidhania wenzangu, roho zao zinatisha,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Wacheka mkikutana, rohoni ni tofauti,
Kifanikiwa wanuna, wataki upande chati,
Roho zao za supana, milele kukaza nati,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Kuna wakabaji koo, hulka zao za chatu,
Waua kama minyoo, ingawa sote tu watu,
Juu ngozi ya kondoo, kumbe ndani mbwa mwitu,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.
Roho mnatoboana, kuvichuma vya dunia!
Hata ngozi mwazichuna, bila kuhisi hatia,
Vibaya mwatendeana, na mali kujipatia,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Jaribu kuwa makini, hepuka kuwa na pupa,
Kuna wapenda madeni, hawapendi kuyaripa,
Wakitia mifukoni, wataanza kukukwepa,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Zapita siku tisini, watoto wataka ada,
Mdeni haonekani, imekuwa kawaida,
Ameingia mitini, mpaka awapo na shida,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Wazee mwanishangaza, hasa ninyi wa makamo,
Watoto mwawatongoza, bila kuwa na kikomo,
Tena mnawapumbaza, kwa kutumia midomo,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

Wengi watu wa heshima, jamii yawaheshimu,
Wana mambo ya kinyama, japo wao wanadamu,
Kila nikiwatazama, wengi hawana nidhamu,
Jione kwenye kioo, uziondoe kasoro.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Dira (Sehemu ya Tano)


Pombe hadi saa sita, uchumi humo kizani,
Wa gongo mwawakamata, hawapandi kizimbani?
Tupige ulevi vita, chanzo cha umaskini,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Waume kwa wanawake, muda mwingi vilabuni,
Kazi wazipiga teke, mchana pombe vichwani,
Watembea kwa makeke, watoto wako njaani,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Tathimini wako moyo, epuka hulka hasi,
Ulafi nao uchoyo, hizi tabia za fisi,
Tabia uliyonayo, ipukutishe kwa kasi,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Wapo pia wanafiki, nduguze ubinafsi,
Akili zao fataki, wapendelea maasi,
Hawa nao tuwamaki, mwenendo wao ni hasi,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Wengi kwenye jumuiya, waendekeza dhuruma,
Mwenendo huu mbaya, wakumba hata yatima,
Wahusika mwone haya, hii sifa ya kinyama,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Na ninyi wenye dharau, pia wapenda ugomvi,
Tabia zetu limau, zichanganywapo na chumvi,
Ziacheni angalau, kabla ya zenu mvi,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Huduma kwao wajane, hakika tuzingatie,
Pamoja tushikamane, majonzi tuwafutie,
Waajiri tuwabane, mafao wawapatie,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Yangu dira mkubali, kwani tumo safarini,
Kumbuka twendako mbali, hasa ninyi wa angani,
Na hizi rai kauli, ziwekeni akilini,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Dira (Sehemu ya Nne)


Tembelea vijijini, ushirikina ni hofu,
Wananchi tambueni, imani hii potofu,
Mauwaji yaacheni, vikongwe wawapungufu,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Wameibuka magangwe, wazee waangamiza,
Wanaoua vikongwe, ni uchawi watangaza,
Chanzo cha hii mizengwe, macho mekundu wabeza,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Wahuni wana magenge, ya madawa ya kulevya,
Vijana msijidunge, na mwepuke kuyachovya,
Msivagae mkenge, jihadhari kimya kimya,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo

Tuwabane wauzaji, na watumiaji wote,
Wengi wako kwenye miji, wawajibishwe popote,
Na wale wadhururaji, wasiyamezee mate,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Dini zatusikitisha, migongano sasa tele,
Katika yetu maisha, mola tumuweke mbele,
Upendo kuudumisha, tuache kuyumba milele,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Imani yetu nchini, kuabudu tuko huru,
Migogoro ya kidini, inaweza kutudhuru,
Kutupokonya amani, kama kuku kwa kunguru,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Dira (Sehemu ya Tatu)


Tuwe macho duniani, na kung’aa kwa mwili,
Kuna walozua fani, iitwayo utapeli,
Mabazazi wa nchini, ndiyo miradi kamili!,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Ona madereva wetu, gari la Umma ni lao,
Kutwa mara tatu tatu, ndilo lao azimio,
Kwa nini wanathubutu, na yupi ni kimbilio?
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Chunguza mali ya Umma, nasi ututaarifu,
Waipitisha kwa nyuma, mwaita wabadhirifu,
Sheria itawazima, kwani pia waharifu,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Kila mtu augua, kwanini mnashangaa?
Wagonjwa mwawabagua, eti mwaona kinyaa,
Yawabidi kutambua, si utu kunyanyapaa,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Zichunguze zetu kaya, utafumba macho yako,
Mwisho utaona haya, kwa hayo maangaiko,
Wanyanyasika vibaya, kisa virusi ni mwiko,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Dira (Sehemu ya Pili)


Najua unaelewa, mola hutoa umbile,
Wapo walopungukiwa, na hawakupenda vile,
Msiwaache wakiwa, na kuwatenga milele,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Walemavu kuwajali, ndiyo iwe yetu jadi,
Misaada mbalimbali, wapeni wao zaidi,
Kwao tusiwe wakali, katu tusiwakaidi,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Ona watoto yatima, wanaranda mitaani,
Hawana baba na mama, waona giza mbeleni,
Siwapite wima wima, nilichonacho wapeni,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo

Maisha yana utata, maringo yako ya nini?
Mbele sawa na karata, wathamini maskini,
Si vizuri kuwaita, watoto wa mitaani,

Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.
Wapo wagangao njaa, bila ya utaratibu,
Wazunguka kama saa, bila hata wajibu,
Si kila kinachong’aa, ukadhania dhahabu!,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Dira (Sehemu ya Kwanza)


Tumo ndani ya bahari, tunaongozwa na dira,
Abiria jihadhari, akijalizwa king’ora,
Majini kuna hatari, waweza pata hasara,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Hebu ndege tazameni, Dira ndiye  Kiongozi,
Ingawa kuna rubani, bila dira haiwezi,
Kweli tumo safarini, hili naliweka wazi
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Elimu ni kama dira, itutowayo gizani,
Ili tuzidi kung’ara, popote ulimwenguni,
Ujinga una madhara, waleta umaskini,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Wanafunzi na Walimu, na wanavyuo wenzetu,
Zingatieni elimu, Dira ya vizazi vyetu,
Wanazuoni kwa zamu, tufunze jamii zetu,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Dira (Sehemu ya Kwanza)


Tumo ndani ya bahari, tunaongozwa na dira,
Abiria jihadhari, akijalizwa king’ora,
Majini kuna hatari, waweza pata hasara,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Hebu ndege tazameni, Dira ndiye  Kiongozi,
Ingawa kuna rubani, bila dira haiwezi,
Kweli tumo safarini, hili naliweka wazi
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Elimu ni kama dira, itutowayo gizani,
Ili tuzidi kung’ara, popote ulimwenguni,
Ujinga una madhara, waleta umaskini,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

Wanafunzi na Walimu, na wanavyuo wenzetu,
Zingatieni elimu, Dira ya vizazi vyetu,
Wanazuoni kwa zamu, tufunze jamii zetu,
Hii ndiyo dira yetu, kubali wake mwongozo.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Dukuduku (Sehemu ya Pili)


Pindi wana-kukirimu, lengo lao walijua?
Utajihisi muhimu, mabaya hutodhania,
Maneno yao matamu, fisadi hutong’amua,
Kwa fadhira za msimu, baadae wajutia,
  Takrima ni adui, sawa na kidudu mtu.

Chujio likiwadia, koboko naye ni mwema,
Watu atuzawadia, bila kuleta kiama?!,
Siku akijishindia, katu hatoi huduma,
Anyata kwa kudundia, huku sumu akitema,
  Takrima ni adui, sawa na kidudu mtu.

Usiku wabisha hodi, takrima mkononi,
Wajifanya ni zawadi, eti wanakuthamini!,
Kwa mtizamo jadidi, wana siri kibindoni,
Wakugeuze mradi, siku hizo za usoni,
  Takrima ni adui, sawa na kidudu mtu.

Hakika hii si ofa, bali ni hofu yaleta,
Wa hivi wanakifafa, wana-kaya mtasota,
Baadaye ni maafa, wenyewe mtayapata,
Mwapaswa kuziba nyufa, msijejenga ukuta,
  Takrima ni adui, sawa na kidudu mtu.

Yatupasa kuwabeza, mbeleni watatukwaza,
Takrima yatutweza, wazalendo twapooza,
Hebu jaribu kuwaza, kabla ya kujiponza,
Kwani chema chajiuza, kibaya chajitembeza!
  Walimwengu tuwe macho, kuepusha dukuduku

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Dukuduku (Sehemu ya Kwanza)

Nami nalodukuduku, nalo ukera mtima,
Ingawa sijajishuku, chombo chaenda mlama,
Maneno kama chiriku, siyo chanzo cha neema,
Uchezaji wa mapiku, waipunguza rehema
  Walimwengu tuwe macho, kuepusha dukuduku.

Kamtindo kamezuka, wenye kura kukirimu,
Wale tuliopevuka, huu siyo ukarimu,
Ona pirikapirika, wote wataka kudumu,
Kwa wanaokurupuka, machoni watiwe ndimu,
  Takrima ni adui, sawa na kidudu mtu.

Dhana yake yapotoshwa, na wale wanaopwaya,
Wengi wetu tumechoshwa, kwa hizo fikra boya,
Wanafaa kunyooshwa, waache kuwayawaya,
Takrima nayo rushwa, kama umeme na nyaya,
  Takrima ni adui, sawa na kidudu mtu!

Kila atowaye kitu, kuna jambo atafuta,
Vichwani ajaza kutu, tudhani ametameta,
Kumbe ana ukurutu, anang’aa kwa mafuta,
Sirika hii ni butu, tunapaswa kuifuta,
  Takrima ni adui, sawa na kidudu mtu.

Kuna kitu wahitaji, kwa kujifanya ni wema,
Njuruku pia vinywanyi, wagawa bila kuhema,
Wapitapo kwenye miji, jembe na chumvi mwachuma,
Watubana kienyeji, pasipo tambua njama,
  Takrima ni adui, sawa na kidudu mtu.

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Kiama (Sehemu ya Pili)

Chunguza kwenye Umati, Uvaaji unatisha,
Picha za uasherati, sinema zinaonesha,
Soma kwenye magazeti, ulimwengu umekwisha,
Chungulia intaneti, vijana zawapotosha,
  Kweli hiki ni kiama, je wangapi watapona?

Chanzo cha ‘homosekisho’, mie chanitatanisha,
Weupe ndio fundisho, kwa nini watudunisha,
Wafrika iwe mwisho, mila zetu zatutosha,
Na tuweke ukumbusho, wanetu kuwafundisha,
  Kweli hiki ni kiama, je wangapi watapona?

Magonjwa sasa asidi, wanadamu hatuoni,
Majanga nayo yazidi, vizazi vi-matatani,
Mazingira twakaidi, jua liko utosini,
Tudumishe tufaidi, la sivyo tumo jangwani,
  Kweli hiki ni kiama, je wangapi watapona?

Ukahaba wanawili, danguro zaongezeka,
Labda wana vibali, nani wakunung’unika?
Ingawaje hatujali, wanafunzi wahusika,
Japo twaficha ukweli, wote tunaadhirika,
  Kweli hiki ni kiama, je wangapi watapona?

Pande nne duniani, tumshujudu manani,
Baibo na Kuruani, zitupe matumaini,
Zinayo hekima ndani, pamoja tujifunzeni
Tusije pata huzuni, duniani na mbinguni,
  Kweli hiki ni kiama, je wangapi watapona?


Sheria zifanye kazi, kwa watiwao nguvuni,
Nawe uliye mzazi, piga upatu bungeni,
Shiriki ngazi kwa ngazi, wafike mahakamani,
Watwaribia vizazi, kwa miigo uzunguni,
  Kweli hiki ni kiama, je wangapi watapona?

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Kiama (Sehemu ya Kwanza)

 Naililia dunia, wapi inaelekea?
Mwovu hutomnunia, kwani atakuchekea!
Mwizi hutomdhania, jinsi anavyoongea!
Shetani amepania, utambi kutuchomea,
  Kweli hiki ni Kiama, je Wangapi watapona?

Nazo nyumba za wageni, sasa hazitamaniki,
Makahaba kwa wahuni, waingizana lukuki,
Yatendekayo gizani, mengi hayasimuliki,
Wakaao vijiweni, kwa bangi hawambiliki,
  Kweli hiki ni kiama, je wangapi watapona?

Mabinti watoa mimba, bado ngono hawaachi,
Watoto wadhani pumba, watupa bado wabichi,
Mola alichokiumba, waondosha kwenye nchi,
Wazidisha kujipamba, kwa kuvaa nusu uchi,
  Kweli hiki ni kiama, je wangapi watapona?

Penzi la jinsia moja, mjini limeshamili,
Jamii yajikongoja, usodoma wavinjali,
Usaganaji si-tija, wapotosha maadili,
Ushoga pia nataja, wamchukiza jalali,
  Kweli hiki ni kiama, je wangapi watapona?

Wanandoa wenye hati, hawadumu kwenye ndoa,
Uzinzi na kurawiti, nasaha zatiwa doa,
Ufumanizi gesti, huko bandika bandua,
Kuvuta mihadarati, dhambini twajongea,
  Kweli hiki ni kiama, wangapi watapona?

Wanaume wafunga ndoa, wanawake vilevile,
Kanisa la shadidia, wawe pamoja milele!
Kwa mola hili ni doa, toka zamani za kale,
Muhimu kuliondoa, lisifikie kilele,
  Kweli hiki ni kiama, wangapi watapona?

Useja pia usimbe, jamii yakumbatia,
Kwenye ulevi wa pombe, vijana watumbukia,
Ushabiki wa kipambe, wagubika familia,
Pasipo mbinu kabambe, taifa laangamia,
  Kweli hiki ni kiama, wangapi watapona?

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Maisha bila Ajira (Sehemu ya Nne)


        Ratiba yangu kwa siku, yasawiti wazi dhiki,
Mara kule mara huku, ndipo nipate riziki,
Mchakato naushuku, kasoro hazitibiki,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Jamaa anilaghai, niendelee kuishi,
Dawa ya mlalahoi, kutumia ushawishi,
Ufukara ni adui, japo mwatia nakishi,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Asubuhi naamka, kichwa chawaza ajira,
Nishie nae kumbuka, ni kaka yake na mama,
Mwenye ukwasi hakika, na kazi ya kumripa,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Kazini anapokwenda, pamoja na mke wake,
Majukumu naachiwa, jamani niwambieje,
Mpate sadiki haya, yanayonipa kiwewe,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Mosi, ninapoamka, magari ninasafisha,
Watoto huwaandaa, shuleni waweze kwenda,
Jinsi walivyodekezwa, mwenzenu nimeshachoka,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Pili, sokoni huenda, mahitaji kununua,
Huko ninaowakuta, wote ni akina mama,
Hakika hunishangaa, sokoni ninapoenda,
Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Nguo zao nazifua, nakupiga pasi pia,
Ifikapo saa saba, shuleni nahitajika,
Watoto kuwachukua, nyumbani kuwafikisha,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Maji yakisha-katika, nahitajika kusomba,
Mengi yameshanikuta, siwezi yote eleza,
Namlilia yehova, shidani kuniepusha,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Hata kidato cha sita, elimu niliyonayo,
Tena gredi ya kwanza, yafaa kuajiriwa,
Popote pale kwa muda, kabla ya chuo kwenda,
Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Singependa fadhaika, na kupatwa matatizo,
Ubongo kutiwa doa, nikiwa kijana bado,
Niepushe uloguswa, leo kwangu kesho kwako!
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Wito nautoa kwenu, mliofanikiwa sasa,
Msinyanyase wenzenu, kwani maisha mlima,
Tuchezeni kama timu, pasipo kubaguana,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Maisha bila Ajira (Sehemu ya Tatu)


Nazifanya jitihada, japo nipate fursa,
Nifukie hizi shida, na kukomesha mkasa,
Sitojitia kidada, ajira nikiinasa,
 Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Naupiga moyo konde, kutokomeza jazba,
Niishi japo kwa kande, kwani ajira haiba,
Ninalia chondechonde, ukosefu wake mwiba,
   Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Subira yavuta heri, mengi nitavumilia,
Wapo watu mashuhuri, shidani walipitia,
Baba MANDELA jasiri, ni mfano asilia,
   Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Ukiritimba ukwasi, wazua danganyatoto,
Matakwa ya wamilisi, hayajali mchakato,
Ahueni mfilisi, ajira bado fukuto,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Nahisi nimepumbazwa, kama mbuzi wa kafara,
Nazidi kugandamizwa, wao shamrashamra,
Busara zangu zapozwa, zisijezua madhara,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Jirani panikinai, kila siku hekaheka,
Ndugu yangu awa ndui, nifanyacho anicheka,
Mizengwe na kujidai, mtaani asikika,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Mafanikio fahari, kwa wale waliovikwa,
Kuajiriwa johari, kwa walokwisha kuchekwa,
Umaskini jeuri, ndiyo kinga ya kubezwa,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Wengine ni wapagazi, waitafuta riziki,
Wapo na mapaparazi, waganga yao ni dhiki,
Usijivune kwa kazi, siku hazitabiriki,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Dunia kweli hadaa, walimwengu ni shujaa,
Utajawa na fadhaa, nawe upate wasaa,
Utalopata balaa, maisha kizaazaa,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Maisha bila Ajira (Sehemu ya Pili)


Kutwa nzima mchakavu, mwana wa kusadikika,
Mambo yanayonisibu, ni vitimbi na pilika,
Nataka fikra pevu, nitoke kufikirika,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Juani nachakarika, shughuli kama Roboti
Rohoni naweweseka, kweli huu Usaliti,
Nyumbani wanapofika, zaanzishwas varangati,
    Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Naota mafanikio, kukwepa hii fitina,
Ajira bado uzio, vijana vichwa twakuna,
Uchumi kisingizio, kwa tulowapa dhamana,
Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Mlezi wangu kumbuka, mkali kama shubiri,
Asubuhi anang’aka, kama mpiga zomari,
Ndugu huyu ni chikaka, asopenda tafakuri,
Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Matusi ya rejareja, kabwela wanitukana,
Moyoni sina faraja, waamka wamenuna,
Wanitendea vioja, siwezi hata kuguna,
Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Mezani anikebehi, utadhani masihara,
Kisa sina maslahi, tumbo latia hasara,
Mwenzenu namsitahi, roho yavuta subira,
Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Nimepatwa masahibu, mithili ya tingatinga,
Naishi kibubu-bubu, nashindwa hata kulonga,
Mwendo huu wa sulubu, mfano wa karandinga,
Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Ndugu ana mushikeli, laiti ningelijua,
Sina mustakabali, nazidi kudidimia,
Maisha kitendawili, yangu faraja bandia,
Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Mwenyeji wangu mchumi, sura ya kihafidhina,
Hila zake za kisomi, mpenda kubaniana,
Mwepesi wa kujihami, kashfa kutupiana,
 Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Sudi yangu maridhawa, sitaki malalamiko,
Napewa ahadi hewa, nisifike niendako,
Usiku najadiliwa, hoja hazina mashiko,
 Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS

Maisha bila Ajira (Sehemu ya Kwanza)

 Naishi Dar es Salaam, maisha ni songombingo,
Ndugu namwona sumu, kwa kuwa ana maringo,
Kwani ameza vitamu, mie kanipa mgongo,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Rohoni sina kinyongo, kwa huu wangu mkosi,
Wapo washika vitengo, watwona vikaragosi,
Wako juu kiviwango, ukianza wadadisi,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Ajira nimetafuta, hadi kwenye Makampuni?
Huko kote sijapata, Urasimu ni Kiini,
Mtaani nimesota, ndugu yangu firauni,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Ndugu niishie kweke, kanifanya hausi-boi,
Kutwa kazi zifanyike, napolala niko hoi,
Ghiliba za mke wake, maseng’enyo hakatai,
  Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

 Nashinda ndani ya geti, utadhani mnyampara,
Nazidi kukaza buti, jijini pamenikera,
Ndugu yangu kizingiti, naishi kama tiara,
   Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Jua kali la utosi, nguo zanukia jasho,
Jamaa ana Ukwasi, mifukoni sina posho,
Sina kazi mahsusi, jijini kwangu kitisho,
   Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Lanikumba sokomoko, pakushika sipaoni,
Kuchapo misukosuko, waishi kisultani,
Naomba mabadiliko, hatilii maanani,
   Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Mwenendo wa kinafiki, jamaa Kabarikiwa,
Tabia za kizandiki, zanifanya kuchachawa,
Nilipo hakukaliki, labda kwa majaliwa,
 Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Fedha zaparaganyika, kweli mie hohehahe,
Lakini sijabweteka, natafuta japo shibe,
Mashaka ya utabaka, yamefanya nizurure,
 Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

Ndugu anapokuona, atembea chapuchapu,
Adhani utambana, akupe marupurupu,
Akugeuza mtwana, shibe yako chupuchupu,
 Maisha bila ajira, nifanyeje walimwengu?

  • Digg
  • Del.icio.us
  • StumbleUpon
  • Reddit
  • RSS